Latest Updates

MARAFIKI, ULIMI WAKO, KABURI LA MAPENZI YAKO-3

MARAFIKI, ULIMI WAKO, KABURI LA MAPENZI YAKO-3

Tunaendelea na mada yetu tuliyoianza siku kadhaa zilizopita. Tunaendelea kuanzia pale tulipokuwa tumeishia.
Upande wa pili, kuna ulimi wako. Kipi ambacho unakitamka kuzungumza na watu? Ni nini unachomwambia mwenzi wako? Kwa pamoja, vitu hivyo, vinaweza kuufanya uhusiano kuanguka kutoka kwenye uimara wake hadi kuwa legelege kabla ya kuvunjika kabisa.



Kasoro kubwa ambayo watu wengi wanayo ni kutochunga ndimi zao siku za mwanzo za kukutana na wapenzi wao. Aghalabu, mtu anakuwa anahisi huyo aliye karibu naye ni wa kupita tu, kwa hiyo anaamua kuzungumza vitu ambavyo baadaye humletea shida. Tena shida kwelikweli!
Nashauri kila mtu awe na nidhamu ya kuzungumza pale anapokuwa na mtu ambaye kuna dalili ya kuingia naye kwenye uhusiano wa kimapenzi. Huwezi kujua utasafiri naye mpaka wapi, kwani wengi wameoana lakini ndoa zao zinaishi kwa staili ya kusutana kila leo, wakikumbushana maneno waliyoambiana nyakati zilizopita.

ZINGATIO LA KISAIKOLOJIA
Nyakati za mwanzo za uhusiano wa kimapenzi, watu wengi huficha kucha. Unaweza kumwambia mwenzio kitu ambacho kinaweza kumfanya aone kinyaa hata kuendelea na wewe lakini asikasirike. Pengine akakuunga mkono au akakushauri kwa lugha iliyotulia.
Hata hivyo, jambo hilo unalomwambia halitakwisha kichwani kwake. Pale atakapokuwa amekuzoea, ataanza kukushusha thamani kila anapokumbuka yale matamshi yako. Juu ya yote hayo, matokeo yake ni kuvunjiana heshima kwa kukumbushana mambo ya kuumiza.
Huumiza kwa sababu pale mwanzoni alipokuwa anazungumza hakuwa na mapenzi ya dhati kama anayoweza kuwa nayo baadaye mapenzi yanapomkolea.
Sasa basi, dawa ni kuchunga ulimi wako ili baadaye usije ukajuta pale utakapokuwa unakumbushwa. Nenda salama, tena tembea juu ya karatasi nyeupe, baadaye utajionea mwenyewe jinsi ambavyo maisha yako ya kimapenzi yanaweza kuwa rahisi na matamu kuliko kawaida.
MFANO; Jane alipokuwa anaanza uhusiano wa kimapenzi na Raja, alidhani mapenzi yao ni urafiki na yatapita tu. Hivyo basi, mwanzoni Jane akawa anaweza kutamka maneno magumu, akiwaambia rafiki zake, huku Raja akisikia. Hakumhofia kabisa kwa lolote.
Siku moja, rafiki yake alimtania, akamwambia: “Usisahau kutumia kondomu, utapata mimba isiyotarajiwa.”
Jane akajibu: “Nikipata mimba ‘naflash’, mbona kitu rahisi?”
Yule rafiki wa Jane akaongeza: “Umezoea eeh, shauri yako?”
Raja ambaye alikuwa anasikiliza yale mazungumzo, alikasirishwa sana na utani ule. Kuanzia pale yule rafiki wa Jane alipoanzisha, maana aliona anamkosea heshima, pili namna ambavyo Jane alijibu, alishangaa sana. Hata hivyo, Raja hakutia neno, alivumilia kwa sababu mapenzi ndiyo kwanza yalikuwa yanaanza.
Siku zilivyokwenda mbele, Raja alimzoea Jane. Sasa akawa na ujasiri wa kuhoji baadhi ya vitu. Siku moja Raja aliumwa na kulazwa kwenye hospitali moja iliyopo Kinondoni, Dar es Salaam. Jane alipokwenda kumwona, akamwambia: “Baby hii hospitali wanatoa sana mimba.”
Raja akashtuka kuisikia kauli hiyo kutoka kwa mwenzi wake, akaiunganisha na ya siku ile alipokuwa anataniana na rafiki yake: “Nikipata mimba ‘naflash’, mbona kitu rahisi.” Vilevile, Raja akayakumbuka maneno ya yule rafiki wa Jane: “Umezoea eeh, shauri yako!”
Hapohapo, Raja akamuuliza Jane: “Wewe umejuaje kama hapa wanatoa mimba?”
Jane akajibu: “Najua tu, si unajua mimi ni mwanamke?”
Raja: “Ukiwa mwanamke ndiyo ujue sehemu za kutoa mimba?”
Jane: “Je, nikisema nimeshatoa mimba hapa?”
Raja: “Hapo unamaanisha wewe ni mzoefu wa kuchoropoa mimba siyo?”
Jane: “Una maanisha nini kuniita mzoefu?”
Raja: “Kauli zako zinatoa picha. Siku ile ulisema ukipata mimba unaflash, leo umefika hapa hata hatujaongea kuhusu ugonjwa wangu, wewe unasema hapa wanatoa mimba. Asimuliaye mvua imemnyeshea.”
Jane: “Labda kama una yako, nisikwambie kitu ninachokijua? Wewe siku hizi una wivu sana.”
Raja: “Jane naanza kupata picha mbaya sana kwako. Huko nyuma ulishanitamkia kuwa wewe unapenda sana ngono, tena ulikuwa mzinzi sana. Na hili la utoaji mimba. Maneno yako yanaonesha wewe ni mwanamke malaya sana.”

MBINU ZA KITAALAM ZA KUDHIBITI USALITI- 2

MBINU ZA KITAALAM ZA KUDHIBITI USALITI- 2

USALITI ni pasua kichwa. Unatesa na kuumiza wengi kwenye mapenzi. Walio ndani ya ndoa na ambao bado hawajaingia. Ni tatizo sugu ambalo kwa hakika linawasumbua wengi.


Ndiyo maana hapa kwenye All About Love tumelipa nafasi ya kulijadili kwa mapana ili tuweze kupambana nalo. Wiki iliyopita nilianza kwa kueleza namna ambavyo mtu anavyotakiwa kwanza yeye kuwa mwaminifu ili kumuweka mpenzi wake katika nafasi ya kumwamini na kuachana na mawazo ya kumsaliti.
Hebu twende tukaone vipengele vingine...
REJESHA NAKSHI ZA MAHABA
Mfano una mashaka mwenzi wako anakusaliti au unamhisi vibaya kutokana na namna alivyo makini zaidi na simu yake kipindi hiki. Lakini inawezekana kabisa, umeshafuma meseji zisizostahili kwenye simu ya mpenzi wako au umepata fununu kwamba anakusaliti.
Kubwa zaidi, inawezekana una ushahidi wa moja kwa moja kwamba anakusaliti. Anatoka na mtu mwingine. Usipaniki maana haitakusaidia, lazima usogee hatua moja mbele.
Huyo ni wako, tayari mpo kwenye ndoa, kuachana haiwezekani na hata kama inawezekana si suluhisho la mwisho, kwani yawezekana ukakutana na mwingine mwenye kasoro zaidi ya huyo.
Kitu cha kwanza kabisa kufanya ili kukomesha usaliti katika ndoa/penzi lenu ni kukumbusha yale ya zamani!
Unajua kuna umri fulani wanandoa wakifikisha, wanajisahau. Wanakuwa hawana jipya; si kwamba hawana jipya, bali hawataki kuonesha mambo mapya.
Nasema wanaweza kufanya mapya kwa sababu mwanandoa huyo huyo anayetoka nje kwa kukosa mapya kutoka kwa mpenzi wake, akienda nje, anakuwa mtundu balaa! Yapo, yanaonekana na watu wanayajua.
Mume ana nyumba ndogo na mke naye ana nyumba ndogo. Ngoma droo! Haina maana kabisa.
Hata kama mwenzi wako hajaanza katabia haka kachafu, lakini ni vizuri basi ukapambana ili kukomesha au kuzuia isitokee.
Wengi hujisahau baada ya kuingia kwenye ndoa, hili ni tatizo. Hebu twende tukaone zaidi.

(i) Kutoka pamoja
Hebu vuta picha, kipindi cha mwanzo wa mapenzi yenu, wewe umependeza na mwenzi wako naye pia, mnatoka pamoja na kwenda kuangalia bendi mnayoipenda, ufukweni au kwenye hoteli ya kifahari...mapenzi yanasonga jamani!
Huwezi kukaa na mkeo kila siku kwenye kochi lilelile, unamtazama kwa mtazamo uleule, halafu ukienda muziki unakutana na mademu wakali, unadata na kusema mkeo hana mvuto. Nani kasema?! Hebu mchukue, mpige pamba halafu nenda katika klabu za usiku, kama hamtagombana na wanaume  wanaomkodolea macho!

(ii) Surprise
Si lazima iwe ya fedha kubwa, kitu chochote kinaweza kuwa surprise. Acha kujidanganya, hebu nunua hata maua ya elfu moja, pulizia manukato safi, halafu mpe ukimwambia; “Nakupenda baby.” Unataka surprise gani zaidi ya hiyo?
Kila anapokuwa anaona zawadi yako, atajihisi mgumu kumkubalia Pedeshee nanilii anayemsumbua kila anapokwenda buchani. Akili kichwani mwako mtu mzima!

(iii) Badili mazingira
Achana na ulimbukeni wa kila siku kukutana na mkeo sehemu moja, mbona zamani mlikuwa mnatoka na kulala nje ya mji au hotelini? Kuna mkono unapofikia, hata ukimchukua mwenzi wako na kwenda naye kwenye hoteli za kawaida bado utakuwa umebadilisha mazingira na utaonekana mpya.
Kumbuka kinachotafutwa hapa ni upya wa ndoa na mapenzi  na kumfanya mwenzi wako asiwe na wazo la kusaka nyumba ndogo.

SAKA MSISIMKO ZAIDI
Ili penzi liendelee kuwa imara lazima utafute msisimko zaidi, yapo mengi ambayo yanaweza kuongeza msisimko katika penzi lako.  Haiwezekani rafiki yangu uwe unarudi nyumbani saa tano usiku kila siku, unadhani utamwona mkeo ana tofauti?
Hapa ni kujidhibiti mwenyewe, maana usipokuwa makini, unaweza kushangaa unamdharau mkeo na kumuona hana mvuto kabisa. Huo mvuto utauona wapi kama kila ukija unamkuta amevaa kanga moja anataka kulala?
Utamuona wa kawaida na mwisho wa siku utaamua kutafuta kitulizo nje, ambapo mapenzi ndani yatapungua na si ajabu na yeye akaamua kusaka mahali pa kupumzisha moyo wake.
Mwanasaikolojia mmoja amewahi kuandika katika kitabu chake kuwa ili uzidi kumuona mpenzi wako mpya kila siku, lazima umfanye rafiki yako nambari wani.
Alisema: “Mke/mume lazima awe rafiki yako wa kwanza, unadhani utamuonaje wa muhimu kwako, kama hampati muda wa kuwa pamoja mkazungumza kirafiki?
“Tunashauri wanandoa wawe na muda wa mzaha, kutoka pamoja, kujadiliana mambo mbalimbali kirafiki ili kujenga ustawi bora zaidi wa ndoa yao.”
Akaendelea: “Huwezi kuwa na mkeo, kila siku yupo kwenye muonekano uleule, akakuvutia. Lazima leo awe amevaa sketi na blauzi, umshike mkono na kwenda naye beach, kesho mmekwenda pamoja Kariakoo kununua mahitaji. Utampenda daima.”
Alieleza kuwa mke kukaa ndani kihasarahasara ni kati ya mambo yanayoua mvuto na ushawishi wa kimapenzi ambao baadaye huzaa nyumba ndogo.
“Utakuta mwanamke akiwa chumbani na mumewe anakaa hovyohovyo, sehemu ya maungo yake yako wazi, sasa nini kitamvutia mumewe kama kila siku anamuona katika hali hiyo? Hapa lazima wanawake nao wawe macho jamani, vinginevyo hizi nyumba ndogo hazitaisha,” aliongeza.
Naamini kuna kitu umejifunza, wiki ijayo nitakuwa hapa katika mwendelezo wa mada hii, USIKOSE!

Joseph Shaluwa ni Mshauri wa Mambo ya Mapenzi anayeandikia Magazeti ya Global Publishers. Ameandika vitabu vya True Love, Let’s Talk About Love na All About Love vilivyopo mitaani.

MARAFIKI, ULIMI WAKO, KABURI LA MAPENZI YAKO

MARAFIKI, ULIMI WAKO, KABURI LA MAPENZI YAKO
MARAFIKI na mpenzi wako ni nani bora? Kabla hujajibu fumba kwanza macho kisha tafakari. Umeshapata jibu? Usijibu, hebu vuta picha kwa mara ya pili, fanya tafakuri ya kina kisha lipime jawabu lako. Kile ambacho umepata ndiyo muongozo wa kila siku katika maisha yako.
Hata hivyo, naomba nikupe changamoto kupitia hilo jibu lako. Kuna kipindi marafiki wanaweza kuwa muhimu kuliko mwenzi wako, vilevile zipo nyakati zikifika, haitawezekana kumpa rafiki kipaumbele kuliko mpenzi wako. Hapa inataka maarifa na akili tulivu kuchanganua.
Rafiki anaweza kuwa muhimu kipindi unamsoma mwenzi wako. Hata hivyo, umuhimu wake una ukomo, kwani hatakiwi kuchukua akili yako au kumpa hata asilimia 50 ya mawazo juu ya kile ambacho unataka kukiamua. Asilimia 15 zinamtosha, kisha zingatia; akili za kuambiwa changanya na zako.
Maisha yako yapo ndani yako mwenyewe. Unachohitaji au kukitamani katika maisha yako ya kimapenzi, unakijua wewe. Kama ndivyo, basi tambua kuwa ukimsikiliza sana rafiki, anaweza kukupotosha. Matokeo yake anaweza kukufanya uishi ndani ya matarajio yake.
Wewe na yeye, kila mmoja ana sifa zake anazoziangalia kwenye mapenzi. Una sifa ambazo unadhani mwenzi wako akiwa nazo maisha yako yatakuwa na furaha, naye anavyo vipengele ambavyo anataraji ‘waubavu’ wake awe navyo ili amani na upendo vitawale.
Mathalan, unaamini kuwa mwenzi wako anapaswa kuwa mtanashati, mzuri wa umbo na sura lakini mwenzako anaamini kwamba vyote hivyo ni sawa lakini kama tabia yake siyo nzuri hafai. Hapo utakuwa umeshaona namna ambavyo wewe na yeye mnatofautiana. 
Unaamini katika mpenzi mwenye mapenzi ya kweli, anayejali, mwelewa, asiye na gubu, mwaminifu, rafiki yako kipaumbele chake ni kumpata mwenye fedha. Hapo ikupe picha kuwa wewe ni wewe na yeye ni yeye. Ukizubaa, utapoteza matarajio yako kwa sababu ya kushikiwa kichwa na rafiki yako.
Ni dhambi kubwa, tena ni usaliti wa hali ya juu kuacha misingi ambayo wewe unaamini inaweza kukupa furaha, utulivu na amani ya moyo na kufuata ushauri wa rafiki yako ambaye hana uwezo wa kusoma hisia zako na kujua nini hasa unahitaji. Atadhani upo kama yeye, kwa hiyo atakwambia ufuate anachopenda yeye.
Ipo mifano ya watu wanaoteseka leo kwa sababu ya kupotoshwa na marafiki. Walikuwa na wapenzi wazuri sana, waliokuwa wanasikilizana nao lakini wakaachana baada ya kushauriwa ndivyo sivyo. Picha iliyo wazi kwa sasa, mapenzi kuwa na vurugu nyingi, ikufanye uelewe mantiki ya hoja ambayo naijenga.
Kama marafiki wenyewe wanachukuliana wapenzi, ni kwa nini isikupe sababu ya kuamini kwamba wewe upo sahihi zaidi kwenye uamuzi wako kuliko mshauri? Pengine akakujaza maneno ya chuki kwa mwenzi wako, mwisho ukamwona hafai, baada ya majuma mawili unagundua yupo naye.
Ukiweka pembeni hoja ya kuchukuliana wapenzi, ukweli mwingine ni kwamba rafiki anaweza kukufanya uachane na mwenzi wako mnayependana na kuelewana vizuri ili ukajiweke kwa mwenye fedha. Mwisho wa hilo siku zote kuna majuto, kwa maana pesa itakuwezesha kutatua mambo mengi lakini haziwezi kukupa penzi linalokidhi moyo.
Kama ambavyo umewahi kushuhudia mateso ya mtu kulazimishwa kuoa au kuolewa na yule asiyempenda kwa sababu mbalimbali, hususan kichocheo cha shinikizo la wazazi, ndivyo hutokea pale uhusiano unapojengwa na fedha. Shika neno hili kuwa binadamu ni rahisi sana kuzizoea fedha pale anapokuwa anazipata.
Anapozoea maisha ya fedha, moja kwa moja humuona wa kawaida sana, yule mwenzi wake aliyemkubali kwa sababu ya mali. Ni hapo ndipo humsaka yule atakayempa tulizo la kweli la moyo. Vitendo vya wenye fedha wengi kusalitiwa, ikupe sababu ya kuyazingatia haya.
Kwa nini baadaye uje kuvuna aibu ya kuonekana msaliti? Amua leo kwamba pamoja na hali yoyote ya kimaisha uliyonayo na mwenzi wako, mtalindana kwa shida na raha. Yote yanawezekana, endapo kwa maelewano yenu na nia ya dhati, mtajitolea kusaka maisha bora zaidi, yatapatikana tu.