Latest Updates

MAKUNDI YA WANAWAKE NA MITAZAMO YAO KWA WANAUME



Ogopa sana mwanamke akikuona wewe ni tatizo, hilo huwa linajengeka na kuishi kwa muda mrefu ndani ya kichwa chake.
Mara chache wanawake ambao huitwa akina mama wa nyumbani, kwa maana ofisi zao ni majukumu ya ndani ya familia peke yake, hujitutumua katika eneo la faragha lakini nao siyo wote. Inapotokea akazaa, ndiyo hushindwa kabisa kuonesha hata yale makeke kiduchu ambayo awali aliyaonesha.




Ukiweka pembeni suala la faragha, wanawake wa kundi hili huwa wanapenda sana. Kwa kawaida,
wakishakita nyoyo zao, huwa hawatazami kwingine. Ni wazuri mno katika kipengele cha kuhimili vishawishi. Wanaweza kusumbuliwa kwa kutongozwa lakini wakabaki imara bila hata kuwashirikisha waume zao.

BAHATI MBAYA 
Wao ni waaminifu lakini kutokana na misimamo yao na kutoyapa kipaumbele mapenzi ya kitandani, hujikuta wakisalitiwa mara nyingi sana. Maajabu yaliyopo ndani yao ni kuwa inawezekana kabisa akajua kwamba mume wake ni msaliti lakini asichukue hatua yoyote, zaidi ya kupigania ustawi wa familia yake.
Wanaweza kukosa tendo la unyumba kwa muda mrefu kutokana na waume zao kuwa ‘bize’ na nyumba ndogo, wakirudi nyumbani wanakuwa wamechoka hata hakuna habari ya kuulizana haki ya ndoa. Maajabu mengine kwa wanawake wa kundi hili ni kuwa wanaweza kunyamaza, wakakaa muda mrefu bila kushiriki tendo bila kuzalisha migogoro ndani ya nyumba.
Wao ni wazalishaji mali, tatizo linalowatesa wanawake wengi wa kundi hili ni kwamba uzalishaji wao, huvunwa na wengine kutokana na tamaa, kiburi na ubabe wa wanaume wao. Hili nalo huvumilia na mara nyingi hujitahidi kupambana na presha ya ubadhirifu wa waume zao kwa ajili ya kuhakikisha maisha ya watoto hayaharibiki.
Janga kubwa zaidi ni kwamba wanawake wa kundi hili huachwa na kusababisha kile ambacho walikichuma, wakakidhibiti kisipotee kwa ajili ya maisha ya kesho, kitumiwe na wengine kiulaini. Sababu kubwa ya wanawake hawa kuachwa pamoja na ukweli kwamba wao ndiyo ‘wife materials’ ni hii;
waume zao husaliti ndoa na kwenda kujirusha na wanawake wa nje (nyumba ndogo), huko hunogewa kiasi kwamba mapenzi yote ya familia zao, huyahamishia nyumba ndogo. Kama hiyo haitoshi, mwanaume huanza makeke mpaka ndoa inapovunjika.
Pindi ndoa inapovunjika, mwanaume humtimua mwanamke kwenye nyumba kisha kujimilisha kila kitu ambacho walichuma pamoja. Mwisho kabisa, mke hubaki hana chochote, akimuacha mwanamke mwenzake akifaidi matunda ya jasho, maarifa na ubunifu wake.
Kitu kikubwa ambacho wanaume huwa hawajui ni kwamba safari moja huanzisha nyingine. Kwamba wanapoanza uhusiano wa nje, hudhani kuwa yatakuwa mapenzi ya juujuu lakini huko nako, hao wanawake huanza kukaba mpaka kivuli, wakitaka haki kuliko wake wa ndoa.
Ni kipindi ambacho wanaume hukosa misimamo na kutetereka. Mke wa nyumbani anamtaka na nyumba ndogo anaihitaji. Mke wa nyumbani huwa hajui kuhusu haya mapambano, kwa hiyo huendelea kuishi maisha yaleyale ya kawaida bila kujua kuwa yanamwathiri.
Nyumba ndogo, yenyewe huongeza makeke kwa sababu inakuwa inajua kuhusu mapambano yaliyopo. Mwisho kabisa, mwanaume huona kwamba mke wa nyumbani hana burudani, kwa hiyo hufanya uamuzi wa kijinga zaidi kwa kuvunja nyumba na kumtimua mke wa ndoa.
Wanaume wengi waliofanya matukio ya aina hii, baada ya miezi michache walijuta, baada ya kubaini kwamba yule aliyemfanya akavunja nyumba yake, hakuwa mwanamke bali gubegube. Pamoja na hayo, ukweli ni kwamba mara nyingi wanawake wa kundi hili hawathaminiki.
Wanawake wa kundi hili ni almasi lakini kwa macho ya kawaida, unaweza kudhani ni chupa.

0 Response to "MAKUNDI YA WANAWAKE NA MITAZAMO YAO KWA WANAUME"

Post a Comment